Adbox

Monday, November 25, 2019

Bodi ya Korosho yawaonya wanunuzi wanaochelewesha fedha za Wakulima

Na Ahmad Mmow-Nachingwea

Bodi ya korosho (CBT) imesema haitawahurumia wala kuwaonea haya wanunuzi wa korosho ambao watachelewesha fedha za malipo ya wakulima wa zao hilo.

 Tahadhari hiyo ilitolewa jana mjini Nachingwea na mkaguzi wa ndani wa bodi ya korosho, Christopher Mwaya ambae alimwakilisha mkurugenzi mkuu wa bodi hiyo kwenye mnada wa nne wa korosho kwa chama kikuu cha ushirika cha RUNALI.

Mwaya alisema wanunuzi hawanabudi kuingiza fedha za wakulima kwenye akaunti za vyama vikuu vya ushirika kwa wakati kwa mujibu wa miongozo kwani serikali haipo tayari na haikusudii kuingia kwenye mgogoro wala lawama na wakulima kuhusu kutolipwa fedha baada ya korosho zao kununuliwa na wanunuzi hao.

Alisema serikali kupitia bodi hiyo haitasita kumchukulia hatua kali mnunuzi atakaye kiuka miongozo kwa kuchelewesha malipo hayo.

Mkaguzi huyo wa ndani alisema wapo wanunuzi ambao wanatabia ya kuichokoza serikali kwa kukiuka masharti, kwa hiyo katika msimu huu wa 2019/2020 wasithubutu kuchelewesha malipo.

Katika hali inayoonesha serikali haitaki utani kuhusu malipo ya wakulima, Mwaya alisema moja ya kampuni zinazonunua korosho ambayo ilichelewesha malipo imeadhibiwa kwa kulipa takribani shilingi 100 milioni ili zifidie hasara kwa wakulima waliocheleweshewa malipo ya mnada husika.

No comments:

Post a Comment

Adbox