Adbox

Thursday, October 24, 2019

Agizo la Waziri Jafo kwa Halmashauri zote nchini

Na Ezekiel Mtonyole, Dodoma

Serikali imeagiza halmashauri zote nchini kuhakikisha hadi ifikapo Novemba 30, mwaka huu ziwe zimefungua akaunti maalumu kwa ajili ya fedha asilimia 10 za mapato ya ndani kwa ajili ya makundi mbalimbali ya wanawake, vijana na watu wenye ulamavu.

Agizo hilo limetolewa Jijini Dodoma na Waziri Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, (TAMISEMI) Selemani Jafo,  wakati alipokuwa anafunga kongamano la wataalmu wa maendeleo ya jamii waliokutana Jijini hapa.

Waziri Jafo amesema agizo hilo alishawahi kutoa lakini halmashauri nyingi hazijatekeleza, na kulazimika kuagiza hadi ifikapo Novemba 30, mwaka huu halmashauri zote 185 nchini ziwe zimefungua akaunti hiyo maalumu.

“Niliwahi kutoa agizo la kutaka halmashauri kufungua akaunti maalumu kwa ajili ya fedha za mikopo kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye ulamavu ingawa kwa sasa sijajua utekelezaji wake ukoje katika halmashauri".

“Lakini sasa naagizo kwa mara ya mwisho ikifika Novemba 30 mwaka huu, halmashauri zote zihakikishe zimefungua akaunti maalumu ambayo fedha zinazotengwa kwa ajili ya mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, na hili ni takwa la kisheria.” amesema Waziri Jafo.

Amesema kitendo cha Kuweka fedha hizo kwenye kapu moja ni  hatari kwa sababu inakuwa ni vigumu  kuzifuatilia ni kama zimeingizwa kwenye jalala huwezi kuzioana kwa haraka matumizi yake, hivyo kama hakuna kikwazo cha kiutendaji basi ifikapo Novemba 30 halmashauri zifungue akaunti maalumu.

Aidha, ameahidi kuangalia namna ya wizara yake kutenga fedha kwa ajili ya wataalamu wa maendeleo ya jamii ambazo watazitumia kwa ajili ya ufuatiliaji na tathimini ya fedha hizo zilitolewa ambazo zimetolewa katika makundi mbalimbali.

Amebainisha kuwa kutokuwa na uwezeshaji huo, itakuwa ni vigumu kwa maafisa maendeleo ya jamii kufuatilia uendelevu wa vikundi vilivyokopa kwani fedha hizo zinatolewa ili kuweza kubadilisha maisha ya wananchi.

Amebainisha kuwa kwa kazi nzuri inayofanywa na serikali ya awamu ya tano,maafisa maendeleo wanapaswa kuisimamia kiufasaha zaidi ili iweze kufikia malengo yale ambayo serikali imekusudia katika kuinua uchumi wa kati wa viwanda.

Amesema ameandaa zawadi kwa halmashauri tano za kwanza  zitakazofanya vizuri katika uchaguzi huo wa serikali za mitaa ofisi yake itatoa zawadi kwa maafisa maendeleo ambao watakuwa katika maeneo hayo kwa ajili ya kusimamia uchaguzi.

Amesema lengo la kufanya hivyo ni pamoja na kutaka kuwafanya watu hao kufanya kazi bila mawazo,hasa ukizingatia kada yao inadharauliwa sana kutokana na kwamba vitu vibaya vyote wanapewa wao ili hali sekta hiyo ni muhimu kwa ajili ya kuleta chachu ya maendeleo hapa nchini.

“Nitatoa maelekezo katika wizara kuhakikisha mnatafutiwa magari kwa ajili ya kuwarahisishia utendaji wenu wa kazi wa kila siku,”amesema Jafo.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya afya Maendeleo ya jamii jinsia wazee na watoto, Idara ya Maendeleo ya Jamii, Dkt John Jingu amesema anaamini baada ya mkutano huu maafisa maendeleo watakwenda kufanya mabadiliko na kuleta maendeleo katika maeneo mbalimbali wanayotoka.

No comments:

Post a Comment

Adbox