Adbox

Tuesday, March 24, 2020

ATCL yasitisha safari zake za nje ya Tanzania

Shirika la Ndege Tanzania (ATCL)  kuanzia Machi 25, 2020 litasitisha safari zake za nje ya Tanzania ikiwa ni  sehemu ya kukabiliana na virusi vya corona.

Kwa mujibu wa taarifa ya ATCL iliyotolewa leo Jumatatu Machi 23, 2020 inaeleza kuwa safari hizo ni  Entebe(Uganda), Bujumbura(Burundi), Hahaya(Comoro), Lusaka(Zambia) na Harare (Zimbabwe).

Kampuni hiyo imesema haitarejesha fedha  badala yake abiria wote wenye tiketi katika safari zilizositishwa wanatakiwa kuwasiliana na ofisi za kampuni hiyo au wakala wa safari za ndege kwa ajili ya taratibu za kubadilisha tiketi hizo ili zitumike  baadaye katika safari zao bila makato.

“Tumesitisha kwa sababu ya matamko na maagizo ya serikali mbalimbali katika nchi tunazofanya safari zetu, matamko hayo ni kufunga mipaka na kupunguza mwingiliano kwa sababu ya corona,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo iliyosainiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa ACTL, Ladislaus Matindi.

“Tutarudisha safari hizo hali itakapoturuhusu. ATCL itaendelea kutoa huduma za ndani japo kwa kupunguza miruko katika baadhi ya vituo kutokana na upungufu wa abiria kipindi hiki cha tahadhali  nyingi.”

Matindi ameahidi kampuni hiyo kuendelea kujali usalama na afya za wafanyakazi, abiria na wateja kwa kupuliza dawa, kusafisha kwa dawa maalumu ndani ya ndege na mikono.

No comments:

Post a Comment

Adbox